Namwogopa Mnangagwa Kuliko Mugabe

Chambi Chachage

Sijui kama kuna ukweli wowote kuwa kama jina lako la ukoo linaanziwa na herufi ‘M’ basi kuna uwezekano mkubwa wa kuwa Rais. Lakini ninapotazama ramani ya Afrika naona kumekuwa na Marais wengi wenye aina hiyo ya majina: Mandela, Mbeki, Mwinyi, Mkapa, Magufuli. Lakini lao nataka kuongelea Marais wawili waliopokezana vijiti kwa mbinde: Mugabe na Mnangagwa.

Hawa walikuwa Makamaradi. Nasikia eti  bado ni Makomredi. Walipigana pamoja kwenye vita vya ukombozi vya Chimurenga ya Pili. Pia walishirikiana katika mauaji ya kimbari ya Gukurahundi.

Ndiyo maana halikuwa jambo la ajabu pale ambapo mmoja wao alipoonekana kama mrithi wa mwenzake katika kiti cha Urais. Lakini kutokana na mazingira ya kutatanisha, urithi huo ilibidi upatikane kwa mapinduzi ya kijeshi ya aina yake. Mapinduzi hewa.

Leo mrithi huyo ajulikanaye kwa jina la utani la Mamba ambalo nalo linaanza na herufi ‘M’ ameripotiwa kuwa ameteua Mawaziri wakiwamo Makomredi wale wale wa Chimurenga na Gukurahundi. Hili linanikumbusha uchambuzi huu wa majuzi wa Profesa nguli:

“Kuhusu mapinduzi ya Zimbabwe ambayo yanatajwa kuwa ya aina yake, sidhani hayo yalikuwa ya kupindua  Serikali au mfumo wenyewe, bali kumshinikiza Mugabe aachie ngazi ili yule ambaye alionekana ataendelea kulinda masilahi ya kundi dogo la watawala na makamanda wa jeshi waliofaidika binafsi ya utawala wa Mugabe liendelee. Wakati tabaka la la watawala linapoona hatari ya kupinduliwa na umma, tabaka-tawala halisiti kumtoa kafara mmoja wao. Na ndiyo kilichotokea Zimbabwe” – Issa Shivji

Japo sitaki kumnanga mtu, napotafakari tunapoelekea kisiasa nadiriki kusema namwogopa sana Mnangagwa kuliko Mugabe.