Sitaomboleza
Rafiki yangu, kamaradi Henry Mapolu
Sijaja kukuzika
Sijaja kukuaga
Sitaomboleza
Sitabubujika
Nimekuja na marafiki zetu
Na makamaradi wetu
Kupokea mchango wako
Kujikumbusha mfano wako
Ewe kamaradi!
Unatukumbusha mengi ya usafi, sio ya ufisadi
Uhongo wa kisiasa uliukata,
Ukaenda wilayani
Udisi wa Mzee Ruksa haukufarijisha,
Ukauficha ukayani
Aha! hili halikuwa geni kwako
Kwani ulijiuzulu Uzuoni,
Ukaenda Urafikini
Mwito wako kuinua uelewa wa proletari
Hukujali kutunikiwa uzamili wa profesari
Ulituachia mabepari-chipukizi
Wakicheza ngoma ya ulimbikizi
Tumefika kukuenzi
Kwa fikra na mawazo yako
Kwa mtazamo na msimamo wako
Na waledi usiotetereka
Uaminifu usiopingika
Wapo kina Adamu na Zakia
‘Bakileki na Bgoya
Karimu na ukarimu wake
Na Kashiwaki namuona pake
Wapo pia Joe na Jenerali
Sio wa wanajeshi
Wa waandishi-wacheshi
Sitaki niwasahau Mwami na mwenzie Masanja
Eti wakijidai wanasosolojia viranja
Qorro wa Karatu
Amefuatana na Msoma Salumu
Aliyekuwa anatusalimu
‘Venceramos! A luta continua’
Ndio kamaradi: A luta continua
Amekuja pia Rameshi
Vijana wakimtania ‘wa Bangladeshi’
Na mwandishi mwenzio Nizari
Aishio nchi-kavu Kariakoni
Akijitambulisha orijino wa nchi-Visiwani
Namuona mheshimiwa Liundi, balozi
Akipambana na mawimbi ya machozi
Na Mzee Butiku amekaa majanini
Unakumbuka tulivyomsumbua ujanani?
Nimemuona rafiki yako wa siku zile za Kivukoni
Mzee wetu, mzee Ngombale wa Kiliwani
Alikuwa anakuulizia juzijuzi
Nipashe za Kamaradi Henry asiye na upuuzi
Sikuwa na ujasiri wa kumkumbushia
Barua yako ya wazi ulomrushia
Uonjo mkali wa kalamu yako katili
‘Ewe kamaradi wangu wa prolitari
Usikubali kupigwa teke na siasa za jemadari’
Kamwe sitosahau unyekekevu na utulivu wako
Kiburi uliepuka kama tauni, jazba zilikuwa geni kwako
Nilipotunga hadithi ya Amina na kijana mwanafalsafa
Nilikuwa nakuwazia wewe na usawa wa yako falsafa
Shati nje ya suruali, na ndara za kanda mbili
Ukiishi katika risachi fleti namba mbili
Yenye kuta pasi picha wala pambo
Isipokuwa Mzee Maksi na madevu yake ya majigambo
Ndugu yangu, rafiki yangu, Kamaradi Henry – mbele sitaenda
Nakuachie salamu za kamaradi chipukizi Sabatho Nyamsenda:
‘Afrika imepoteza mmoja wa makamanda muhimu
katika vita dhidi ya mfumo huu dhalimu …’.
Issa bin Mariam
02/02/2011
Ndugu zangu,
Henry Mapolu ameaga dunia, juzi Jumapili jioni.
Ni kati ya waanzilishi wa Chama cha USARF na jarida la Cheche katika chuo Kikuu cha Dar es Salaam miaka ya 60. Kwa mliopata kitabu cha “Cheche” mtakuta makala / taarifa zake.
Kwa mliosoma kitabu cha Walter Rodney “How Europe Underdeveloped Africa”, mtakuta ametoa shukrani kwa watu wawili: Karim Hirji na Henry Mapolu.
Prof. Shivji anamwelezea Henri Mapolu kama ifuatavyo:-
Henry alichagua kuwa upande wa wanyonge mapema katika maisha yake tukiwa sote Chuo Kikuu, na kushiriki katika vuguvugu la mwamko wa nadharia na itikadi ya Ujamaa kwa mtazamo wa Kimaksi. Baada ya kufuzu shahada ya uzamili, bila kusita, Henry akaacha kazi yake ya uhadhiri chuoni na kujiunga na Kiwanda cha Urafiki kama Afisa Elimu ili aweze kutoa mchango wake kwa kuamsha uelewa wa wafanyakazi na wavujajasho juu ya hali yao halisi. Mimi binafsi ninafarijika kwamba niliwahi kufanya kazi naye kuandika, kukusanya na kuhariri makala ambayo yalichapishwa katika kijitabu kiitwacho ‘Vuguvugu la wafanyakazi Nchini Tanzania’. Maandishi ya Henry Mapolu yataendelea kuwa nyenzo mojawapo katika mapambano ya wavujajasho dhidi ya mfumo katili wa ubepari.
Issa Shivji
30/01/2010
Hakika Afrika imepoteza mmoja wa makamanda muhimu katika vita dhidi ya mfumo dhalimu wa ubepari / ubeberu.
MAPAMBANO YA KUBOMOA NGOME YA UBEBERU YANAENDELEA
Sabatho Nyamsenda
Comments are closed.


Nimeshtuka kupata taarifa hii. Nilipoingia Chuo Kikuu Dar kama mwanafunzi, mwaka 1973, ndipo nilipoanza kumwona na kumsikiliza Henry Mapolu. Alikuwa mmoja wa wanaharakati waliotupa changamoto sisi vijana. Wanaharakati wengine walikuwa akina Issa Shivji, Mahmoud Mamdani, Yash Tandon, Dan Wadada Nabudere, Walter Rodney, Grant Kamenju, Josaphat Kanywanyi, Frank Mbengo, Gilbert Gwassa, Haroub Othman, Walter Bgoya, Kingunge Ngombale Mwiru, na wengine zaidi, kutoka Tanzania, Afrika Kusini, Uganda, na kadhalika. (Kwa vile nimemtaja Kingunge, napenda tu kusema kuwa Kingunge Ngombale Mwiro wa leo si yule wa miaka ile, alipokuwa Kivukoni)
Tulijifunza mengi kutoka kwa wote hao. Henry Mapolu alibobea sana kwenye suala la wafanyazi na uongozi wa wafanyakazi. Kazi aliyoifanya, pamoja na wanaharakati wenzake, ilitupa motisha sisi vijana wa TANU Youth League, na baadhi yetu tulikuwa tulijiunga na naendesha jarida la "Maji Maji," ambalo lilikuwa ndio mrithi wa "Cheche." Kuondoka kwake kunatuachia pengo kubwa, ila mchango aliotoa ni hazina itakayoendelea kuwepo.
Natoa pole kwa ndugu, jamaa na marafiki. Mungu awape nguvu ya kustahimili kipindi hiki kigumu, na amweke marehemu mahali pema Peponi. Amina.