Wakati ile kesi dhidi ya wafugaji katika kijiji cha Vilima Vitatu wilayani Babati imesogezwa mpaka 30 Juni 2008, mgogoro huoumechukua sura mpya baada ya ‘mwakilishi’ wa mwekezaji, Un Lodge En Afrique (ULEA), kutoa kitisho cha aina yake. Inasemekana Mhandisi huyo wa Kifaransa anayesimamia ujenzi wa ‘loji’ ya kitalii alitoa kitisho hicho kwa mmoja wa wanasheria wanaofuatilia kwa karibu mgogoro huo. Tukio hilo lilitokea hivi karibuni wakati mwanasheria huyo alipopita katika eneo husika kuona hali ya wafugaji hao ambao wako katika hatihati ya kuondolewa katika eneo hilo. Mhandisi huyo alinukuliwa akisema:

‘”I have private concession on this land, you are not allowed to pass here, I know who you are, you are the lawyer for the Mang’ati. Next time you come here I’l shoot you. I have copied your car number you will see soon, the villagers knows your car and they are waiting” [Tafsiri: “Nimepewa mamlaka binafsi juu ya ardhi hii, hauruhusiwi kupita hapa, nakujua wewe ni nani, ni yule mwanasheria wa Wamang’ati. Ukija hapa tena nitakupiga risasi. Nimenakili namba ya gari lako na utakiona, wanakijiji wanalijua gari lako na wanasubiria.”]

Tukio hili limezua mjadala mkali miongoni mwa wanaharakati wa haki za ardhi. Moja ya maswali wanayojiuliza ni, je, kama tayari kuna vitisho vya aina hii nini kitamzuia mwekezaji asitekeleze makubaliano ya kuwaruhusu wafugaji wachunge mifugo katika eneo hilo la malisho kama watahamisha makazi yao? Swali lingine wanalojiuliza ni, je, wananchi wataruhusiwa kupita katika eneo hilo lililo karibu kabisa na ufukwe wa Ziwa Manyara na ambalo ni moja ya njia za kwenda ziwani? Maswali ya aina hii yanazidi kuibuka katika maeneo mengi yanayoingiliwa na wawekezaji kama vile maeneo yaliyopo pembezoni mwa Ziwa Natronna Ziwa Victoria Nyanza.