Hasira ni Udhaifu

Hasira hazijengi, wahenga walitwambia

Mbona sasa huzitengi, mwenzangu wazikumbatia

Tena kwa makeke mengi, bila hata kujutia

Hasira ni udhaifu

Ulitongoza kwa pole, huku ukinyenyekea

Ahadi tele na tele, na nyimbo kuniimbia

Nikakuchagua tule, dume nimejipatia

Hasira ni udhaifu

Ndoa ya kisheria, dunia ikashangilia

Mizinga na zumaria, vyote wakatupigia

Wadini walihudhuria, baraka kutupatia

Hasira ni udhaifu

Ndani tumeingia, hasira waniletea 

Hila zimekuingia, kila kitu wakemea 

Vitisho wanitishia, tena kwa kunionea 

Hasira ni udhaifu

Wanangu wawachukia, waziwazi wawambia

Vita wawatangazia, eti adabu kuwatia 

Huku ukiwatambia, ubabe ulojitwalia 

Hasira ni udhaifu

Wewe si mume wa kwanza, wanne wametangulia 

Ubabe utakuponza, wana watakuchukia

Hakika watakubeza, dharau kukujazia

Hasira ni udhaifu

Ulezi ni kuwafunda, pale wanapokosea

Kwa mapenzi bila inda, heshima utajijengea

Nasi tutakupenda, mapenzi kufurahia 

Hasira ni udhaifu

Hasira ni udhaifu, si sifa wala ujanja 

Watu kuwatia hofu, kamwe hutakidhi haja

Waonesha upungufu, wa ubaba wenye tija 

Hasira ni udhaifu

Unanipa fadhaiko, ndoani mtikisiko

Kucha huishi vituko, vyenye kuleta sikitiko

Walitafuta anguko, maafa mtiririko

Hasira ni udhaifu

Nakuomba kwa hisani, acha ubabe wako

Amani ilete ndani, nifaidi mke wako

Watoto wawe furahani, Jenga familia yako

Hasira ni udhaifu

@Mwanahamisi ‘Mishy’ Singano

Comments Off on Hasira ni Udhaifu