Hitaji Kuu La Mtoto Yatima

Je, ni malazi?

Ama ni mavazi?

Au ni madawa?

Labda ni chakula?

Pengine ni elimu?

Yote hayo muhimu – tena sana!

Ila lipo lingine adimu!

Hitaji la kumbatio.

Kumbatio la upendo.

Kwenye kituo cha kulea watoto yatima wapatao 90 cha CHAKUWAMA pale Sinza (Meeda) karibu na ‘Kanisa (la Full Gospel) la Kakobe’ utakutana na watoto wadogo ambao wala hawatakuomba zawadi yoyote zaidi kupokea ‘kumbatio la upendo’.

Ukimkumbatia mmoja kwa bashasha, mwingine atakuja kwa tahadhari na kukuambia “na mimi”, ukiwakumbatia wote wawili, wa tatu naye atakujia; ukimweka mmojawapo chini, atakuegemea kwa tashwishi uendelee kumkumbatia. Hilo ndilo hitaji la ‘kumbatio la upendo’.

Hiki ni nini, mtoto mmoja yatima aliwahi kumuuliza mtu aliyetembelea kituo fulani cha watoto yatima na kumkumbatia kwa dhati. Mtoto hakujua kumbatio ni kitu gani. Huu unaitwa upendo, mtu huyo alimjibu mtoto yule. Ndiyo, ni  ‘kumbatio la upendo’.

Sambaza ‘kumbatio la upendo’.