
Suluhisho mmojawapo la matatizo yetu ni kuhakikisha kuwa hatuvipotezi na hivyo 2 tulivyo navyo maana tayari nguvukazi inapungua kwa sababu tunapoteza watu kupitia maradhi sugu, ajali holela na kadhalika. Na pia tunapoteza ardhi kupitia uwekezaji uchwara na uporaji. Utafiti wa Bajeti ya Kaya wa hivi karibuni unaonesha jinsi gani familia zetu zinavyoathiriwa na upungufu wa chachu kuu za maendeleo.
Lakini hilo suluhisho mmojawapohaliwezi kupatikana bila kutatua tatizo la ukosefu wa hivyo vitu vingine 2 vilivyobakia, yaani siasa safi na uongozi bora maana hivi tukiwa navyo ndipo tutaweza kudhibiti upotevu wa watu na ardhi. Na kamwe hatuwezi kuwa na utawala bora bila kuwa na uongozi bora. Hivyo, tuiangalie upya siasa yetu ya uongozi na mfumo wetu wa utawala.
Swali la msingi tunaloweza kujiuliza ni kama Usafi wa siasa na Ubora wa uongozi vinategemeana. Na kama vinategemeana kipi kinamtegemea mwenzake.
Kwa mtazamo wangu siasa inategemea uongozi kwani ni viongozi wanaotengeneza sera za maendeleao na ilani za uchaguzi na vitu vingine vinavyoathiri siasa.
Lakini ukiangalia tena uongozi bora unategemea watu kwani viongozi ni watu na ukiwa na watu bora unapata viongozi bora wanaoweka siasa safi na kufanya nchi iwe na uongozi bora.
Kwa hiyo bado tunarudi kwa watu na swali la kujiuliza hapo ni kwamba tunafanyaje watu wetu kuwa bora ili wanaposhika hatamu za uongozi wawe viongozi bora wenye kuendesha siasa safi?