Kisa cha Wananchi Walioibagaza Demokrasia

Chambi Chachage

@Udadisi

Sijui kwa nini leo nimekikumbuka tena kisa nilichohadithiwa na Bibi yangu, Mkunde wa Maore, nikiwa mdogo. Kinahusu watu waliokombolewa kutoka utumwani. Maisha yao mapya hayakuwa na watawala wa kiimla waliowazoea. Wakiwa na migongano walienda kwa waamuzi waliowasuluhisha hadi wakapatana.

Lakini siku moja wakaja juu wakidai na wao wanataka kuwa kama wenzao wa nchi jirani. Walichoshwa na waamuzi wapya ambao hawakuwa kama mwamuzi aliyewapa mikoba. Badala ya kuamua kwa haki, walikula rushwa na kupindisha hukumu ili wafaidike.

Kwa hakika ni sababu ya msingi kabisa kutotaka mafisadi wawe waamuzi. Lakini badala ya kutafuta waamuzi wazuri ili waendelee na mfumo huo huo ambao kwa kiasi kikubwa ulikuwa umegatua madaraka na hivyo kuwa wa kidemokrasia zaidi, wao walitaka mfumo wa kifalme. Eti mtoto akililia wembe mpe. Ila mwonye.

Basi mwamuzi wao mstaafu akakubali kwa shingo upande kuwatafutia mfalme. Ila akashauriwa awaonye. Bahati nzuri maonyo hayo yamerekodiwa katika historia yao. Yanasema:

“Mfalme atakayewamiliki ninyi atakuwa na desturi hii; atatwaa wana wenu na kuwaweka kwake, kwa magari yake, na kuwa wapanda farasi wake; nao watapiga mbio mbele ya magari yake. Naye atawaweka kwake kuwa maakida juu ya elfu, na maakida juu ya hamsini; na wengine atawaweka walime shamba lake, na kuvuna mavuno yake, na kufanyiza zana zake za vita, na vyombo vya magari yake. Na binti zenu atawatwaa kuwa wafanyaji wa marhamu, na wapishi, na waokaji. Atatwaa makonde yenu, na mashamba yenu ya mizabibu, na ya mizeituni, yale yaliyo mazuri sana, ili awape watumishi wake. Naye atawatoza ushuru wa mbegu zenu na wa mizabibu yenu, awape maakida wake, na watumishi wake. Atawatwaa watumishi wenu na wajakazi wenu, na ng’ombe zenu walio wazuri sana, na punda zenu, naye atawatia katika kazi zake mwenyewe. Atawatoza fungu la kumi la makundi yenu; nanyi mtakuwa watumwa wake. Nanyi mtalia siku ile kwa sababu ya mfalme wenu mliyejichagulia.”

Maonyo hayo hayakufua dafu. Wakaendelea kulilia wawe na mfalme mmoja wa kuwaamua na siyo waamuzi wengi. Tunataka “kuwa na mfalme juu yetu”, wakasisitiza, “ili sisi nasi tufanane na mataifa yote; tena ili mfalme wetu atuamue, tena atoke mbele yetu na kutupigia vita vyetu.” Sauti ya wengi ikawa sauti ya Mungu.

 Huo uhuru wao wa maoni ukaheshimiwa. Ikawa wengi wape. Demokrasia hiyo waliyoichoka na hata kuibagaza ndiyo ikawapa kile kile walichokitaka. Wakasahau kuwa kuna wakati bibi na babu zao walishawahi kuwa chini ya himaya ya kifalme na kitumwa. 

Wananchi hao wakajipatia Mfalme wao. Muda si mrefu wakaanza kulalamika mno. Yale yote waliyotahadharishwa kuwa yatatokea yakatokea. Lakini ndiyo hivyo tena, mfumo wa kifalme ukadumu.

Usiniulize kwa nini nimekumbuka kisa hiki. Nimeshajibu. Sijui.