Riwaya hii ya Majeruhi wa Mapenzi inayotarajiwa kuchapishwa hivi karibuni imemkumbusha Udadisi kuhusu zile riwaya maarufu za Euphrase Kezilahabi na Ben Mtobwa. Japo riwaya ya Rosa Mistika -Waridi Lenye Fumbo (Mystic Rose) aliyoandika Kezilahabi ilikuwa ni riwaya ya mapenzi, ilisawiri jamii ya Kitanzania ya enzi zile kwa mapana yake. Hata ile riwaya ya kipelelezi ya Ben Mtobwa iitwayo Mikononi mwa Nunda nayo ilijaribu kuisadifu jamii kwa upana wake. Zote pamoja na kugubikwa na mfume dume zilijitahidi kutoa taswira ya jamii ambayo mfumo dume wake hujeruhi wanawake (pamoja na wanaume pia) na kuwafanya kuwa majeruhi wa mapenzi wenye visirani na visasi vikali vya kuwafanya nao wawe ‘wajeruhi wa mapenzi’. Katika kipindi hiki ambacho jamii yetu inajihoji kuhusu mahusiano baada ya msiba mkubwa iliyoupata ni muhimu waandishi wetu wakaandika riwaya zinazogusa suala hili kwa kina. Ni matumaini yangu kuwa riwaya hii mpya ya Mzee Mwanakijiji ni zaidi ya mapenzi!