Tutakuombea Mwalimu

Zidumu fikra zako Mwalimu,

Vitabuni na vyuoni.

Sisi wafuasi wako Mwalimu, 

Tutakuenzi kwa vitendo na vituko,

Kwa dhati na fataki.

  

Tutakuenzi Mwalimu,

Kwa kukujengea sanamu,

Kwa kukutengenezea filamu.

Kwa kukujengea kasri ya makumbusho.

Pasi jasho wala posho.

Tunakuenzi Mwalimu,

Kwa kukarabati fikra zako mgando, ziwe za kisasa.

Tunakuenzi Mwalimu,

Kwa kuugeuza wako mwelekeo, kwa kupiga msasa,

Uwe freshi wa karne ya leo, kufiti enzi za kisasa.

Tutakuenzi daima,

Tutakuombea milele,

Makanisani na miskitini.

Ulale usingizi fofofo wa milele,

Makaburini na mbinguni.

Amen.

Issa bin Mariam

24/08/2014