UTENZI WA MIAKA 50 YA UHURU (BETI 100)

Home>Archive>UTENZI WA MIAKA 50 YA UHURU (BETI 100)

SIFA KWA MUNGU!

1. Ee Mola ninakujia

Kwako ninasujudia

Sifa nakurudishia

Utukufu enzi pia

2. Ewe uliye Jalia

Mmiliki wa Dunia

Hukumu ni zako pia

Na adhabu ya Jehania

UTANGULIZI

3. Kalamu naishikia

Naandika beti mia

Kwa tungo nazipangia

Zinasifu Tanzania

4. Ni tungo za historia

Ni wapi tulianzia,

Na wapi tumefikia,

Lengo ni kukumbushia

5. Nataka kusimulia

Kwa hizi tungo mia

Huku nawahisabia

Mpaka zitapotimia

6. Tangu walipoingia

Wageni toka Asia

Na wale wa Yuropia

Makabila yalohamia

7. Ishirini na mia,

Makabila ya Tanzania,

Makubwa madogo pia

Hapa nawasimulia

8. Na beti zikitimia

Zikifika hizo mia

Kalamu nitaachia

Lengo nitalifikia.

9. Ujumbe nauanzia

Wa hizi beti mia

Kwa kina nitagusia

Ni wapi tulianzia

FUNGUA LINKI HIZI UENDELEE KUUSOMA:

http://groups.yahoo.com/group/Wanazuoni/message/13009

au

http://www.jamiiforums.com/jukwaa-la-siasa/199846-utenzi-wa-tanzania-miaka-hamsini-ya-uhuru-beti-100-a.html

MTUNZI:

Na. M. M. Mwanakijiji (Sauti ya Kijiji)
Disemba 5, 2011
Email: mwanakijiji@jamiiforums.com
Facebook: “mimi mwanakijiji”

Ω

USULI:

Nilipata wazo la kuandika utenzi huu* kuanzia mwaka jana. Nilikuwa nimekusudia kuandika Utenzi wenye beti 1000 kwa ajili ya maadhimisho ya miaka 50 ya Uhuru wa Tanzania. Lakini katika uvivu wangu na mihangaiko ya dunia nimejikuta nimeishia kwenye hizi beti 100 za utenzi huu wa Tanzania. Maadhimisho ya miaka hamsini ya Uhuru ni maadhimisho siyo ya mipaka ya nchi, siyo ya jina na kwa hakika kabisa siyo maadhimisho ya kupita kwa muda. Ni maadhimisho – naamini- ya utu wetu.

Kwamba, katika miaka hamsini iliyopita tumeweza kufanya kile ambacho hakikuwahi kufanywa kwa miaka 2000 iliyopita katika eneo letu. Yaani, kuwaunganisha watu watu wetu wote, chini ya mipaka ile ile, wakiwa huru na haki sawa. Katika utenzi huu nimeelezea jinsi eneo letu lilivyojulikana kama Azania katika masimulizi ya Wagiriki au kama Zenji kwa Waarabu na wakati mwingine kuhusiana na majina ya maeneo ya Kushi na Nubia katika Biblia. Kama jamii ya watu tumepitia mambo karibu yote ambayo yamepitiwa na jamii nyingine za dunia. Kuanzia maisha ya ujima, utumwa, vita, mapigano, na hatimaye uhuru.

Kumbe basi historia yetu haina tofauti sana na historia ya jamii nyingine za watu ambazo zimesimama katika pande za dunia. Unaposoma utenzi huu ni matumaini yangu utakufanya ujisikie fahari kuwa wewe kama vile mimi ni zao la historia hii. Tumefungamanishwa na historia kiasi kwamba haiwezi kufunguka. Mbele yetu wametutangulia wengi katika historia ambao nao walisimama kutambua utu wao na kuudai mbele ya watawala wa zama zao. Ni hiki ndicho tunachokifurahia kwamba leo tuko huru kuwa watu sawa na wengine – kwa kila hali.

Ni utu wetu ndio ulikuwa msingi wa kupigania uhuru wetu na unatakiwa kuwa ndio kiini cha kushangilia uhuru huo. Ni vipi tumetumia uhuru huo kuinua utu wetu hili ni swali jingine ambalo kizazi chetu kama kizazi kinachokuja kitahiji kujibu. Je, mambo tunayoyafanya na kufanyiana yanalingana na utu huo? Je, tunatendeana kama watu wenye utu katika sera, sharia, mipango, na mambo tunayoyafanya? Utenzi huu basi ni kukumbushia utu wetu.

MMM Disemba 5, 2011

2021-05-28T02:33:44+03:00

About the Author:

Assistant Professor and founder of @Udadisi/Profesa Msaidizi na Muasisi wa @Udadisi - https://udadisi.com/chambi-chachage/ Akaunti ya Twita/Twitter Handle: @ChambiChachage
Go to Top