Wakuu

Muhidin J. Shangwe

(@ShangweliBeria )

Imeibuka tabia, ya kuitana Wakuu

Ishakuwa kuu kadhia, hadhi kuwekana juu

Nijuze wapi lianzia, neno la wakati huu

Limeenea mitandaoni, kila mtu Mkuu!

Ujuzi sifa yao, kila jambo walijua

Mtandaoni ndo’ kwao, japo pote huyazua

Zamani na mamboleo, Wakuu wasochagua

Nabaki na moja swali, heshima au kujitutumua? 

Wakuu mmetanabahi, kwamba fulani fisadi

Kigogo mpiga dili, ramli kwa ripoti ya Assadi, 

Tena mwapiga zumari, Si wa kwanza wala pili,

Nazongwa kujiuliza, Wakuu ’kina nani?

Wakuu twashukuria, kwa wenu uzalendo

Habari kutupatia, japo maneno si vitendo

Nasi twaaminia, kuupenda wenu mtindo

Habari hizi nyeti, Wakuu mwazipata wapi?

Imekuwa kama desturi, kwa hizi mpya zama

Kwa ubaya na uzuri, utukufu kuuparama

Japo matendo sifuri, kutwa kucha kulalama,

Waungwana kuitana Wakuu, ni heshima au woga?

Kaditama mefika mwisho, melonga pasi ficho,

Kweli yaja mwisho,Tena haihofu tisho,

Hongeraye mvunja zungusho, Tena pasi fukisho,

Kifiwacho Kiswahili, au fikiri za Waswahili?