“Ukimgusa Mwanamke Umegonga Mwamba” – Wanawake Wapigania Uhuru wa Afrika Kusini

Bibi yangu mzaa mama anaitwa Mkunde. Bibi yake mzaa mama alijulikana kama Shode. Hivyo huyu Bibi yangu aweza kuitwa Mkunde Binti Orupa Mwana Shode.

Kisa cha maisha ya wanawake hawa ni kiungo muhimu katika historia ya familia yetu. Kwa kiasi kikubwa wamekuwa mwamba ama msingi ambao mama yangu, Demere, amejijenga. Kile walichokifanya wote hawa ni mhimili mkubwa katika maisha yetu.

Orupa Mchikirwa alimlea Mkunde katika kipindi ambacho Wakoloni na Wamishionari walikuwa wameingia katika Milima ya Upare ama Vuasu kama ijulikanavyo katika lugha ya Chasu. Kilikuwa ni kipindi kigumu katika jamii za Kiafrika. Sina hakika kwa nini walimuita Mchikirwa yaani aliyezirwa. Ila ni hakika jina la Orupa lilitokana na yule Orpa aliyekataa kwenda nchi ya ugenini pamoja na mkwewe Naomi kwenye kile Kitabu cha Biblia cha Ruth. Mkulu Orupa hayupo nasi kimwili leo ila bado ni nguzo yetu. Kumbukumbu yake hutusaidia kudumisha udugu.

Sijawahi kujumuika katika kusanyiko lolote la wajukuu, vitukuu , vining’ina au vilembwe vya Mlala Orupa Mchikirwa ambapo hatajwi. Kwa kiasi kikubwa yeye ndiye aliyekuwa mama wa mama yangu, dada na kaka zake pamoja na binamu zao. Pamoja na shida kubwa zilizokuwa zikimkabili bibi huyu mjane bado alihakikisha kuwa walio wake hawalali na njaa. Hata wageni wake alihakikisha wanashiba pia.

Inasemekana wakati hali ya ukame ilipozidi na ugumu wa maisha kumuelemea alifunga ‘mshanga’, yaani kamba, kiunoni ili apunguze makali ya njaa na aweze kulima kwa ‘kikumbu’, yaani, kijembe chake, ili kuwe na chakula nyumbani kwake.

Chakula kichache alichokuwa nacho hakukila bali aliwaachia wanawe na wajukuu zake. Yeye alibaki na mshanga na kikumbu tu mchana kutwa. Wale wajukuu wamekuwa madaktari, marubani, walimu na kadhalika. Mchango wake wanautambua.

Katika udogo wangu nililelewa na Bibi yangu Mkunde. Maisha yake hunifanya nitambue urithi alioachiwa na Orupa Mchikirwa. Ustahimilivu. Upendo. Utu.

Ninapowaangalia dada zangu, Mkunde na Rehema, bado nauona urithi huo. Japo tu kizazi cha nne kutoka kwa Koko Orupa Mwana Shode bado hatujapoteza mizizi yake.

Dunia inapozidi kujikita kwenye unyama nitauenzi urithi huu wa ‘Ujamaa ni Utu’.